Header Ads Widget

BENKI YA CRDB, WADAU WA KILIMO WAZINDUA HUDUMA YA MIKOPO YA ZANA ZA KILIMO KWA WAKULIMA

Kushoto ni Afisa Masoko wa Kampuni ya ETC Agro, John Joseph na Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui wakimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko mfano wa funguo ya trekta wakati wa uzinduzi wa za huduma ya mikopo ya zana za kilimo  uliofanyika katika benki ya CRDB tawi la Shinyanga leo Jumanne Septemba 22,2020.  Kushoto ni Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi Said Pamui, kulia ni Meneja wa Benki ya CRDB, Luther Mneney. Wa pili kulia Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Shinyanga, Luther Mneney.  Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akizungumza wakati wa Uzinduzi wa huduma ya Mikopo ya zana za kilimo kutoka Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ya kilimo ‘ETC Agro,Agricom na Loan Agro
Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi Said Pamui akiwakaribisha wakulima binafsi,kutoka kwenye vikundi kukopa zana za kilimo kwani hakuna masharti magumu kama dhamana.
Muonekano wa sehemu ya Matrekta ambayo wakulima wanaweza kukopa 
Muonekano wa sehemu ya Matrekta ambayo wakulima wanaweza kukopa 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akikata utepe wakati wa uzinduzi wa mikopo ya zana za kilimo. Kushoto ni Afisa Masoko wa Kampuni ya ETC Agro, John Joseph. Wa kwanza kulia ni Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui akifuatiwa na Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Shinyanga, Luther Mneney.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko akijaribu kuendesha trekta wakati wa uzinduzi wa mikopo ya zana za kilimo. 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) na Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui wakifurahia jambo baada ya kupanda kwenye matrekta wakati wa uzinduzi wa huduma ya mikopo ya Zana za Kilimo.Katikati ni Meneja wa Benki ya CRDB Tawi la Shinyanga, Luther Mneney.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimkabidhi funguo ya Trekta Mkulima kutoka Bariadi mkoani Simiyu Malugu Masanja Nshashi (kushoto) aliyenunua trekta kwa njia ya mkopo kupitia Benki ya CRDB. Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimkabidhi funguo ya Trekta Mkulima kutoka Bariadi mkoani Simiyu Manjobola Mome (kulia) aliyenunua trekta kwa njia ya mkopo kupitia Benki ya CRDB.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko akipiga picha ya kumbukumbu na viongozi wa benki ya CRDB, Kampuni ya ETG Agro na wakulima kutoka Bariadi mkoani Simiyu walionunua matrekta kwa njia ya mkopo.
Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo ya kilimo ‘ETC Agro,Agricom na Loan Agro wamezindua huduma ya Mikopo ya zana za kilimo yakiwemo matrekta kwa wakulima ili kuwawezesha kukopa kwa riba nafuu bila kuweka dhamana ya ziada ili kuboresha kilimo chao.

Uzinduzi wa Mikopo ya zana za kilimo umefanyika leo Jumanne Septemba 22,2020 katika Benki ya CRDB tawi la Shinyanga ambapo Mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo wa mikopo ya zana za kilimo, Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Mhe. Jasinta Mboneko aliipongeza Benki ya CRDB kwa ubunifu wao wa mara kwa mara katika kurahisisha uboreshaji wa maisha ya Watanzania kiuchumi na hasa katika kuunga mkono juhudi za serikali kuondoa umaskini wa kipato kwa wananchi wake.

“Benki ya CRDB mmetia fora katika sekta ya kilimo,wakati wa msimu wa pamba napo mlishiriki kikamilifu kutoa fedha na leo mmekuja na mikopo ya zana za kilimo,yakiwemo matrekta haya tena bila dhamana za ziada”,alisema. 

Mboneko alieleza kuwa matrekta hayo yatawasaidia wakulima kuboresha kilimo chao badala ya kutumia jembe la mkono na majembe ya kukokotwa na ng’ombe ili kuongeza uzalishaji hivyo kilimo kuwa na tija zaidi.

"Naomba wakulima mchangamkie fursa ya kununua matrekta yaliyotolewa na Benki ya CRDB kupiti wadau ambao ni ETC Agro (wauzaji wa matrekta ya Mahindra), Agricom (wauzaji wa matrekta ya Swaraj na Kubota) na Loan Agro (wauzaji wa matrekta ta John Deer)”,alisema Mboneko.

“Hongereni sana Benki ya CRDB,Mara zote CRDB mmekuwa wabunifu wa kushiriki kwa karibu katika miradi mbalimbali ya kimkakati ya serikali yetu hasa kwa kipindi hiki ambacho Tanzania ipo katika uchumi wa kati”,aliongeza Mboneko.

Mkuu huyo wa wilaya aliwataka wakulima,vyama vya msingi vya mazao (AMCOS),wakulima binafsi hususani wa zao la pamba,mpunga na alizeti kuchangamkia fursa ya mikopo ya zana za kilimo ili kuhakikisha kilimo chao kiwe na tija zaidi.

Kwa upande wake, Meneja wa Benki ya CRDB Kanda ya Magharibi, Said Pamui alisema benki ya CRDB kwa kushirikia na Makampuni ya uuzaji matrekta ‘ETC Agro,Agricom na Loan Agro’ wameboresha taratibu za utoaji wa mikopo ya zana za kilimo kupitiaa benki ya CRDB ili kuwawezesha wakulima kukopa bila kuweka dhamana ya ziada kwa riba nafuu.

Alieleza kuwa benki ya CRDB imeamua kuleta wadau wa maendeleo ya kilimo ili kuwapunguzia wakulima riba kubwa na kupata mikopo ya dhana za kilimo bila kutumia hati za nyumba ambapo pia matrekta yatakuwa yanafanyiwa matengenezo na wauzaji hao wa matrekta.

“Benki ya CRDB ni benki ya Kimkakati inayounga mkono jitihada za serikali kuwaongezea kipato wananchi na imekuwa ikishirikiana na serikali bega kwa bega kutekeleza miradi ya kuwaletea maendeleo wananchi na imechangia nchi kufikia uchumi wa kati”,alisema Pamui.

Aidha alisema benki ya CRDB, ni benki ya wananchi na inaongoza kuwa karibu wakulima na kwamba hatarajii kuona wakulima wanaendelea kulima kizamani kwa kutumia majembe ya mikono ama ya kukokotwa na ng’ombe.

Naye Afisa Masoko wa Kampuni ya ETC Agro, John Joseph alisema kupitia mikopo ya zana za kilimo,kinachotakiwa kufanywa na wakulima ni kutoa mchango wao katika ununuzi wa trekta usiopungua 25% ya bei ya trekta.

Katika uzinduzi huo wa huduma ya mikopo ya zana za kilimo,Mkuu wa wilaya ya Shinyanga,Mhe. Jasinta Mboneko amekabidhi matrekta kwa wakulima wawili kutoka Bariadi mkoani Simiyu ambao ni Njobola Ng’weleja Mome na Malugu Masanja Shashi.

Post a Comment

0 Comments