Header Ads Widget

WAZAZI WATAKAOOZESHA WANAFUNZI KUCHUKULIWA HATUA KALI

Mwenyekiti wa Mtaa wa Dome Kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga. 

Wazazi wanaoishi katika mtaa wa Dome manispaa ya Shinyanga mkoani hapa, ambao watabainika wameozesha watoto wao wa kike na wa kiume watachukuliwa hatua kali za kisheria.
   
Baadhi ya wanafunzi wa Shule za Sekondari Manispaa ya Shinyanga

                                      Na  Suzy Luhende Shinyanga Press Cub Blog
Hayo yamesemwa na mwenyekiti wa mtaa wa Dome Solomon Nalinga kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika  katika Mtaa huo, ambapo amesema wazazi watakaobainika kuwa wameozeshwa, wazazi watachukuliwa hatua za kisheria kwani watoto wote wana haki ya kutimiza ndoto zao. 

Nalinga amesema wazazi wote wanatakiwa wawe wawazi wapeleke taarifa za watoto katika ofisi ya mwenyekiti wasikae na kuficha ukweli waweke wazi taarifa za watoto, ili watoto waweze kusaidiwa na wandelee na masomo kama kawaida. 

“Kama kutakuwa na kiashiria kuwa kuna mwanafunzi ameozeshwa na mtoto haonekani shuleni mzazi utatueleza  ukweli ili watoto wetu tuwajengee mazingira mazuri waendelee na masomo”alisema Nalinga. 

Pia alisema kuna wimbi la wanafunzi wamekuwa wakikatiza mitaani huku wakiwa wamenyoa kiduku na kuvaa nguo za ajabu, suruali za ajabu lakini wazazi wanaona kama fasheni lakini ni hatari kubwa kwa watoto hao. 

“Mkumbuke mara baada ya corona kuna maisha, mara baada ya corona kuna elimu, wale watoto tunahitaji waweze kuwa viongozi wakubwa katika taifa hili iwe vijana wa kike au vijana wa kiume, wazazi tuacheni masihara kwa watoto wetu”alisema Nalinga. 

Aidha alisema baadhi ya watoto ambao hawalali majumbani mwao wanaenda kulala kwenye chumba kimoja ambacho kina viashiria vya watoto wa kike wanaenda kulala humo zaidi ya binti mmoja na vijana wanakuwepo ndani huku wazazi wanaelewa tatizo hilo lakini wanakaa kimya.

Baadhi ya wazazi akiwemo  Elizabeth Mwandu na Joseph Jilala wamesema tatizo hilo lipo kinachotakiwa wazazi wasijisahau na kuwaachia huru watoto wao wa kike na wa kiume, kwani ukiwaachia huru watafanya mambo wanayoyajua wenyewe hali ambayo watashindwa kuendelea na masomo.