Header Ads Widget

BENKI YA NMB YATOA MSAADA WA MASHUKA, MAGODORO NA VITANDA HOSPITALI YA KAHAMA

 Meneja wa Benki ya NMB wa Kanda ya Magharibi , Sospeter Magesse (katikati) akimkabidhi kitanda Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga kwa ajili ya Hospitali ya Manispaa ya Kahama.

Na Mwandishi wa Malunde 1 blog - Kahama
Benki ya NMB Kanda ya Magharibi imetoa msaada wa vitanda vya kujifungulia wajawazito , kulala wagonjwa, magodoro, machela, shuka na viti vya wagonjwa katika hospitali ya halmashauri ya Manispaa ya Kahama Mkoani Shinyanga vyenye thamani ya shilingi Milioni 6.7. ili  kuboresha huduma za afya kwa wananchi hususani wanawake wanaofika kujifungua katika hospitali hiyo.

Akikabidhi vifaa hivyo leo Alhamisi Oktoba 21, 2021 Meneja wa Benki ya NMB wa Kanda ya Magharibi , Sospeter Magesse amesema benki ya NMB itaendelea kuunga mkono juhudi za serikali katika kutatua changamoto kwenye sekta za afya na elimu ili jamii kupitia faida wanayopata iweze kupata huduma bora.

Amevitaja Vifaa vilivyotolewa na benki ya NMB kuwa ni vitanda vya kujifungulia akina mama wajawazito viwili na vya kulalia wagonjwa 4 magodoro 4 , shuka 25 , viti vya wagonjwa vya kusukuma viwili  na machela 2 vyote vikiwa na thamani ya shilingi  Milioni 6.7.

Ameeleza kuwa katika mipango yake, Benki ya NMB  itaendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na serikali katika kutatua changamoto mbalimbali kwenye sekta za afya , elimu kwa kutoa misaada mbalimbali ya kijamii kutoka sehemu ya faida inayopata.

 "Benki ya NMB ikiwa sehemu ya wadau wa maendeleo wakubwa itaendelea kusaidia sekta hizo. Tunatambua kuwa Benki ya NMB inatumiwa zaidi na wananchi katika huduma zake mbalimbali hivyo itaendelea kutumia faida yake inayopata kurudisha kwa jamii kwa kutoa misaada ya kijamii katika kuunga mkono juhudi zao katika suala la maendeleo",amesema Magesse.

Akipokea vifaa hivyo na kukabidhi kwa uongozi wa hospitali ya Manispaa ya Kahama, Mkuu wa wilaya ya Kahama  Mhe. Festo Kiswaga  amesema serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan inatambua mchango mkubwa wa benki ya NMB katika masuala mbalimbali ya maendeleo na kuwaomba waendelee kuunga mkono jitihada hizo.

Kiswaga amesema msaada huo umetolewa muda muafaka kwa sababu hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama imekuwa ikielemewa na wagonjwa kutokana na kuhudumia watu kati ya laki tano mpaka sita kwa wiki huku upande wa akina mama wanaofika hapo kujifungua kwa siku ni kati ya 45 hadi 60.

Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Athuman Juma amesema benki benki ya NMB imekuwa wadau muhimu katika kusaidia sekta ya afya na kuhusu vifaa walivyotoa vitasaidia kupunguza changamoto katika sehemu ya kutoa huduma kwa upande huo.
Meneja wa benki ya NMB wa kanda ya Magharibi , Sospeter Magesse akitoa hotuba alipokuwa akikabidhi msaada wa vifaa katika Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama.
Meneja wa benki ya NMB wa kanda ya Magharibi , Sospeter Magesse akitoa hotuba wakati akikabidhi msaada wa vifaa katika Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama.
Mkuu wa wilaya ya Kahama Festo Kiswaga akitoa hotuba wakati anapokea vifaa vya hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama .
Meneja wa benki ya NMB tawi la Kahama ,Gadiel Sawe akizungumza wakati Benki ya NMB  ikikabidhi msaada wa vifaa kwenye hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Kahama .
Meneja wa benki ya NMB wa Kanda ya Mgharibi , Sospeter Magesse akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Kahama Festo Kiswaga (kushoto)  vitanda , magodoro , mashuka , viti vya wagonjwa kutoka benki ya NMB. Kulia ni Meneja wa benki ya NMB wa tawi la Kahama Gadiel Sawe akifuatiwa na Meneja Mahusiano Serikali na Benki ya NMB Kanda ya Magharibi Bi. Vivian Nkhangaa.
 Meneja wa Benki ya NMB wa Kanda ya Magharibi , Sospeter Magesse (katikati) akimkabidhi kitanda Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga kwa ajili ya Hospitali ya Manispaa ya Kahama
Mkuu wa wilaya ya Kahama Mhe. Festo Kiswaga akiwa amekaa kwenye moja ya viti vya wagonjwa vilivyotolewa na Benki ya NMB

Post a Comment

0 Comments