Header Ads Widget

BABA ASHIKILIWA KWA KUMBAKA BINTI YAKE WA MIAKA 13 BAADA YA KUTENGANA NA MKEWE


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba

Na Damian Masyenene –Shinyanga
VITENDO vya ukatili wa kijinsia na matukio ya ndoa za utotoni kwa wasichana wadogo mkoani hapa yanazidi kuripotiwa, ambapo Jeshi la Polisi mkoa wa Shinyanga linamshikilia mzazi aitwaye Petro Maro (43) kwa kosa la kumbaka mtoto wake wa miaka 13 ambaye ni mwanafunzi wa darasa la saba.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari mjini Shinyanga leo Septemba 29, 2020, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba amesema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 27, mwaka huu saa 5:00 asubuhi katika Mtaa na Kata ya Kambarage, Manispaa na Mkoa wa Shinyanga, ambapo mama msamalia mwema aligundua mtoto huyo kubakwa na baba yake mzazi wakati binti huyo akiwa amelala usiku.

Kamanda Magiligimba ameeleza kuwa chanzo cha tukio hilo ni tamaa za kingono baada ya mtuhumiwa kutengana na mama mzazi wa mtoto huyo kitendo kilichopelekea kuishi na mtoto huyo.

Ambapo, ACP Magiligimba ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi ili kukomesha matukio hayo ya ukatili dhidi ya watoto na hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayejihusisha na matukio hayo.

Tukio hilo linajiri zikiwa zimepita takribani siku 15 baada ya Jeshi hilo kuwashikiliwa watu wanne mkoani hapa kwa tuhuma za kumuozesha binti ambaye ni mwanafunzi wa darasa la tano katika Shule ya Msingi Samuye wilayani Shinyanga mwenye umri wa miaka 12 kwa mahari ya ng’ombe wanane na Sh 600,000.

Ambapo tukio hilo lilitokea Septemba 14, mwaka huu saa 12:40 jioni katika Kijiji cha Isela Kata na Tarafa ya Samuye wilayani Shinyanga, jambo ambalo linazidi kurudisha nyuma juhudi za kutokomeza matukio ya ukatili na ndoa za utotoni kwa wasichana mkoani hapa.

Post a Comment

0 Comments